PATA POWER BANK ZENYE UBORA WA HALI YA JUU KWA BEI NAFUU ZAIDI

PATA POWER BANK ZENYE UBORA WA HALI YA JUU KWA BEI NAFUU ZAIDI

Wednesday, October 31, 2012

SERIKALI YAJA JUU MAFUTA KUADIMIKA



SERIKALI imeagiza Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (Ewura), kuchukua hatua za kisheria dhidi ya kampuni zote zitakazokaidi kuuza mafuta kwa sasa, hali iliyosababisha usumbufu mkubwa kwa wananchi.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi alitoa tamko hilo jana Dar es Salaam baada ya kupokea taarifa ya Ewura na Kampuni inayoratibu uagizaji wa mafuta wa pamoja (PIC) iliyoonesha kuwa kuna akiba ya mafuta inayotosha kutumika kati ya siku 10 na 14.
“Hatuwezi kuona wananchi wanateseka wakati kuna mafuta ya kutosha nchini, wale ambao hawataki kuuza chukueni hatua haraka,” alisema Maswi.

Awali, Mkurugenzi wa Petroli wa Ewura, Godwin Samwel alipoulizwa sababu za kukosekana kwa nishati hiyo, ambako ilielezwa kuwa jana baadhi ya mikoa haikuwa na nishati hiyo kabisa, alijitetea kuwa ni kweli mafuta yapo.
Samwel alifafanua kuwa uhaba huo umetokana na kampuni kubwa kuamua kuuza mafuta hayo kwa vituo vya kampuni zao na kuvikatalia vituo ambavyo havina kampuni kubwa kununua mafuta hayo, hali ambayo imezua kizaazaa cha mafuta nchini huku mikoani hali ikiwa mbaya zaidi.

“Ndio maana utakuta vituo vingine vina mafuta na vingine havina,” alisema Samwel na kutaja sababu nyingine ya upungufu huo kuwa ni kuwepo meli zinazopakua mafuta ya kwenda nje ya nchi na migodini kwa muda mrefu katika boya la KOJ wakati meli zenye mafuta ya ndani zikisubiri.
Naye Mwenyekiti wa Bodi ya PIC, Shaniff Mansour alisema hadi juzi jioni kiasi cha mafuta kilichopo nchini kilikuwa dizeli lita milioni 34.1, petroli lita milioni 20.6, jet 1 lita milioni 15.6 na mafuta ya taa lita milioni 5.2.
Mansour alisema kiasi hicho cha mafuta kinatosha kutumika ndani ya siku 10 na akaongeza kuwa kuanzia jana meli nyingine yenye mzigo wa mafuta imeanza kupakua mafuta katika boya la KOJ ambako dizeli ni tani 23, 700 na petroli ni tani 14, 800 hali inayozidi kuongeza upatikanaji wa bidhaa hiyo.
Mansour pia alisema mafuta ambayo yako nchini yakisubiri kusafirishwa nje (Transit) ya nchi ni mengi zaidi kuliko mafuta ya ndani na akataja kuwa mafuta ya nje; dizeli ni lita milioni 46.6, petroli lita milioni 31.3 na jet 1 ni milioni 4.9 na mafuta ya taa ni lita milioni 1.2.

Kutokana na hali hiyo, mbali na kuwabana wanaosusa kuuza mafuta, Maswi aliagiza Serikali ichukue nusu ya mafuta yanayosafirishwa nje ya nchi ili yatumike hapa nchini.
“Naagiza kampuni ziuze mafuta mikoani na hata vituo ambavyo havina kampuni mama viuziwe mafuta kupunguza tatizo hili,” alisema Maswi na kuitaka Ewura kuhakikisha magari ya mikoani yanapakia mafuta kwenye maghala yalikohifadhiwa mafuta.
Aliisisitizia Ewura kuwa kampuni ambayo haitaki kuuza mafuta ichukuliwe hatua haraka.
Alitaka pia agizo la kuuza mafuta yaliyokuwa yanasafirishwa nje lianze kutekelezwa haraka na akashangaa kuwa haijawahi kutokea mafuta yanayosafirishwa nje yawe mengi kuliko yanayotumika ndani ya nchi.

No comments:

Post a Comment