PATA POWER BANK ZENYE UBORA WA HALI YA JUU KWA BEI NAFUU ZAIDI

PATA POWER BANK ZENYE UBORA WA HALI YA JUU KWA BEI NAFUU ZAIDI

Sunday, July 7, 2013

Vurugu za Machinga na Polisi Manzese.


Dar es Salaam. Mapambano kati ya Polisi na wafanyabiashara ndogondogo, maarufu Machinga, katika eneo la Manzese, yamesababisha kizaazaa na kusababisha uharibifu wa mali na kufungwa barabara, kusimamisha shughuli zote kwa zaidi ya saa tatu.

Hali hiyo ilitokea baada ya ‘Wamachinga’ ambao waliondolewa kwenye maeneo yasiyoruhusiwa kwa biashara wakati wa ziara ya Rais Barack Obama wa Marekani nchini, kuamua kurejea kwa nguvu katika maeneo hayo.

Shughuli za kijamii na kibiashara katika eneo la Manzese, zilisimama kwa takriban saa tatu kutokana na eneo hilo kugeuka uwanja wa vita na usalama wa wananchi wasiokuwa na hatia kuwa shakani.

Awali polisi walitoa tangazo la kuwataka Machinga hao kuondoka katika eneo hilo agizo ambalo halikuwe za kukubaliwa, jambo lililosababisha kutumika kwa mabomu ya kutoa machozi.

Tukio hilo la Polisi kutumia mabomu hayo lilianza saa 7 mchana hadi saa 9.45, waliposimamisha kutumia mabomu ambayo yalikuwa yakifyatuliwa kuwatawanya Machinga hao.

Wakati Polisi wakizunguka kuwatawanya, machinga nao walikuwa wakiweka mawe na magurudumu ya magari barabarani kuhakikisha magari ya askari hao hayapati nafasi ya kupita.

Mitaa ya kuzunguka eneo hilo ambalo mara nyingi huwa na mkusanyiko wa watu, lilionekana kuwa wazi huku Polisi wakilitawala kwa kuzunguka huku na kule kuhakikisha zoezi hilo linafanikiwa.

Mwananchi Jumapili lilishuhudia gari la polisi aina ya Land Rover likiwa limejaa wafanyabiashara hao waliokamatwa wakati wa kuwaondoa eneo hilo, ambalo ni kandokando ya barabara inayojengwa ya mabasi yaendayo kasi ya Strabag.

Baadhi ya wafanyabiashara wenye maduka, walijifungia ndani ya maduka yao kuepuka wizi ambao ungeweza kutokea.

Taarifa zinaeleza kuwa baadhi ya mali ambazo zimeharibiwa katima vurugu hizo pamoja na kuchomwa moto kwa jengo la tawi la Klabu ya Yanga eneo la Manzese.

Baada ya barabara kufungwa kwa mawe na wamachinga hao, hali hiyo ilisababisha foleni na usumbufu kwa wenye magari, waliokuwa wakitoka Ubungo kwenda Karikaoo na wale waliokuwa wakitoka Karikoo kwenda Ubungo iliwabidi kutumia njia za vichochoro kuepuka vurugu hizo.

Wakati polisi wakifyatua mabomu hayo, baadhi ya watu walikuwa wakikimbia ovyo huku watoto wakilia bila ya kupata msaada wa kuwaondoa katika eneo hilo.
Baadhi ya watu walilazimika kupanda juu ya Daraja la Manzese ili kukimbia mabomu ya Polisi yaliyokuwa yakilipuliwa mfululizo kuwatawanya wafanyabiashara hao.

Askari hao walifyatua mabomu hayo katika mikusanyiko yoyote, bila ya kujali hata wale waliokuwa katika sehemu za baa na migahawa wakipata vinywaji na chakula.

Mfanyabiashara Steven Frank akizungumzia tukio hilo alisema, Polisi wametumia nguvu za ziada kuwatawanya kitendo ambacho kama wangetumia njia ya kistaarabu wangeweza kutekeleza agizo hilo.

“Palikuwa hakuna sababu ya kufyatua mabomu yao ovyo, kwani sisi hatukuwa tunawapiga wala nini lakini wao wanafyatua tu bila mpango,” alisema Frank.

Mwananchi Jumapili alimsikia mmoja wa Polisi hao akiwasilia na mwenzake kuwa kama wamemaliza mabomu kuna mengine yapo ndani ya gari.

“Kuna katoni kama tatu hivi katika gari, hivyo kama mtamaliza tutawasiliana ili tuweze kuwaongezea, lakini inatubidi tufyatue tu kuwatawanya huku tukiimarisha ulinzi na usalama wa wananchi,” alisikika Polisi aliyekuwa amevaa kiraia.

Kamishna wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alipotafutwa kuzungumzia suala hilo alisema hana taarifa zozote.

Alimtaja Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, Camilius Wambura kwamba ndiye anayeweza kuzungumzia suala hilo. Hata hivyo Wambura alipotafutwa hakuweza kupatikana.

Mmoja wa wafanyabiashara wa eneo hilo, Bashir Zacharia alisema tukio hilo limewasikitisha kwani hawana sehemu ya kwenda ambayo watafanya biashara kwa wingi.